Serikali ya Marekani imetoa Ksh.16 bilioni kuunga mkono juhudi za Kenya za kukabiliana na ukame ambapo Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), limesema fedha hizo zitasaidia kukidhi mahitaji ya dharura kwa takriban watu milioni 1.3 kote nchini Kenya. 

Msaada wa ziada wa fedha hizi kwa ajili ya chakula kwa Kenya, unakuja huku kukiwa na ukame unaoendelea ambao umewaacha zaidi ya watu milioni nne katika hali mbaya ya njaa, huku idadi hiyo ikitarajiwa kuongezeka hadi zaidi ya milioni tano ifikapo Juni mwaka huu. 

Baada ya msimu wa tano wa mvua kushindwa katika Pembe ya Afrika, mvua nyingi nchini Kenya sasa ni chini ya asilimia 70 ya wastani wa miaka 30 kote nchini – na kuzidisha mahitaji ya kibinadamu. 

Rais wa Kenya William Ruto na Mkewe Rais wa Marekani Jill Biden baada ya ziara ya siku 3 nchini Kenya.

USAID itatoa chakula cha dharura kama vile mtama, mahindi, mbaazi za njano zilizogawanyika, na mafuta ya mboga kwa familia zinazoishi katika maeneo ambayo masoko ya ndani hayafanyi kazi. 

Zaidi ya hayo, katika maeneo ambayo masoko yanafanya kazi, washirika watatoa usaidizi wa pesa taslimu kwa familia.

Wakala huo, pia utasaidia mipango ya kuzuia na kutibu utapiamlo kwa watoto, kwani zaidi ya watoto 970,000 wenye umri wa miaka mitano na chini wana utapiamlo wa hali ya juu nchini kote.

 “Kwa kuzingatia ukubwa wa mzozo uliopo, hata hivyo, ufadhili zaidi utahitajika ili kukidhi mahitaji ya kibinadamu yanayotarajiwa hadi mwaka wa 2023,” USAID iliongeza. 

Rais wa kenya, William Ruto amekaribisha tangazo hilo ambalo linakuja kufuatia ziara ya mke wa Rais wa Marekani Jill Biden nchini humo. 

Katika ukurasa wake wa Twitter, Ruto alielezea shukrani zake kwa msaada huo huku nchi ikikumbwa na ukame mbaya zaidi kutokana na miaka 4 ya mvua iliyofeli. 

“Shukrani kwa serikali ya Marekani kwa msaada huu wa ukarimu kwa watu wanaostahili na wanaokabiliwa na ukame mbaya zaidi kutokana na mvua, tunahitaji uvunaji wa maji ili kuimarisha uzalishaji wa chakula/mifugo na kudhibiti athari za mabadiliko ya hali ya hewa, ” Ruto alisema.

Tarimba aibuka tena sakata la mkataba Young Africans
Mashabiki Real Madrid wamuwashia moto Alaba