Kocha Mkuu wa Simba SC Robert Oliviera ‘Robertinho’ amekiri bado kikosi chake kina tatizo la umaliziaji, licha ya kuendelea kuvisimamia vipaumbele vyake kwa kuhakikisha timu inacheza vizuri na kupata ushindi.

Robertinho amesema anatambua bado kuna tatizo katika safu yake ya ushambuliaji, na ndio maana anaendelea kupambana kutatua tatizo hilo, ambalo linaonekana kuwa kikwazo kwenye Benchi lake la Ufundi na kwa Mashabiki kwa ujumla.

Hata hivyo Kocha huyo kutoka nchini Brazil amesema, pamoja na kukabiliwa na tatizo la umaliziaji, bado kikosi chake kimeonyesha kuimarika siku hadi siku, na ndio maana iliwawezesha kupata matokeo katika Uwanja wa ugenini dhidi ya Vipers SC, katika Michuano ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika.

“Pamoja na ushindi ugenini lakini bado tuna tatizo katika eneo la mwisho. Baadhi ya nafasi tunazotengeneza zinapotea hilo linamuumiza kila mtu kati yetu na tunaenda kulifanyia kazi licha ya kwamba tumeshajua wapi tunaanzia,”

“Katika mashindano yote tuliyopo tunahitaji mabao, hususani haya ya CAF ndio tunahitaji kufunga zaidi kwani inaweza kufika sehemu mkalingana alama na mwenzako na kitakachoamua kinakuwa ni mabao”

“Hivyo lazima tufanye kazi juu ya hilo, wachezaji wote kwa pamoja tutawaeleza mahitaji yetu na faida za kupata mabao na mwisho tutaenda kwenye uwanja wa mazoezi kutekeleza hilo kwa vitendo.” amesema Robertinho

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 62, hadi sasa ameiongoza Simba SC kwenye michezo sita, mitatu ya Ligi Kuu na mingine mitatu ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika na kufunga jumla ya mabao sita ambayo ni wastani wa bao moja kwa kila mchezo.

Simba SC kwa sasa inajiandaa na mchezo wa Kombe la Shirikisho Tanzania Bara ‘ASFC’ dhidi ya African Sports ya Tanga, utakaopigwa Jumamosi (Machi 04), jijini Dar es salaam.

Baada ya mchezo huo, Simba SC itakuwa na kazi ya kupambana na Vipers SC kwenye mchezo wa Kundi C, Ligi ya Mabingwa Barani Afrika Jumanne(Machi 07), katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

ikimalizana na mchezo huo, Simba SC kitafunga safari ya kuelekea Morogoro katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kuikabili Mtibwa Sugar, itakayokuwa nyumbani Manungu Complex (11, 2022).

Itakapotoka mkoani Mirogoro, Simba SC itaanza maandalizi ya mchezo wa Mzunguuko watano wa Kundi C, Ligi ya Mabingwa Barani Afrika, kwa ajili ya kuikabili Horoya AC itakayofunga safari kutoka nchini Guinea.

Mchezo wa Mzunguuko wa kwanza wa michezo ya Kundi C, ligi ya Mabingwa Barani Afrika uliozikutanisha timu hizo katika Uwanja wa Jenerali Lansana Conte, ilishuhudiwa Simba SC ikikubali kufungwa bao moja kwa sifuri.

Mkuu wa Wilaya akataa mazoea kazini
Harmonze aomba msaada madai ya pesa zake