Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa  wahakikisha wanatokomeza uvuvi haramu katika ziwa Victoria.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na viongozi wa mkoa huo katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya kikazi mkoani Mara.

“Kuna tatizo kubwa la uvuvi haramu katika Ziwa Viktoria. fanyeni doria za mara kwa mara na watakaobainika hatua stahiki za kisheria zichukuliwe dhidi yao.”amesema Majaliwa

Amesema viongozi hao wanatakiwa wahakikishe wanatokomeza uvuvi haramu haraka iwezekanavyo na pia wasimamie ulinzi wa rasilimali za ziwa Victoria ili ziweze kuwanufaisha wananchi wa mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

Aidha, amesema kuwa baadhi ya wavuvi wamekua wakivua kwa kutumia nyavu zilizopigwa marufuku, kokoro pamoja na mabomu jambo ambalo haliwezi kuvumilika kwa sababu zana hizo zinaharibu uhai wa viumbe hai ndani ya ziwa Victoria.

Hata hivyo, amesema kuwa ni vema mkoa huo ukaanzisha operesheni za mara kwa mara  katika ziwa Victoria kwa lengo la kuwasaka watu wote wanaojihusisha na vitendo vya uvuvi haramu na kuwachukulia hatua kali za kisheria kwa wote watakaokamatwa.

Wajasiliamali watakiwa kuchangamkia fursa
Mpina akitwanga faini kiwanda cha Sanflag