Klabu ya Mtibwa Sugar imetamba kuwa tayari kwa mchezo wa Mzunguuko wa 19 wa Ligi Kuu Tanzana Bara dhidi ya Mabingwa watetezi Young Africans.

Mchezo huo utakaopigwa kesho Jumamosi (Desemba 31) katika Uwanja wa Manungu Complex mkoani Morogoro, utashuhudia Mtibwa Sugar wakisaka ushindi, baada ya kupoteza dhidi ya Ihefu FC kwa mabao 3-1 mwishoni mwa juma lililopita, huku Young Africans wakijipanga kuendelea kufanya kile walichoifanyia Azam FC Jumapili (Desemba 25).

Afisa Habari wa Mtibwa Sugar Thobias Kifaru amesema kikosi chao kipo tayari kupambana na Mabingwa watetezi, na wanatarajia kuwa mchezo huo utakuana upinzani mkubwa kutokana na kila upande kuhitaji matokeo mazuri.

Amesema wanakubali wamekua hawana matokeo mazuri dhidi ya Young Africans kwa misimu ya karibuni, huku akikumbushia namna walivyoteza dhidi ya Wananchi msimu uliopita kwenye Uwanja wao wa nyumbani, lakini akasisitiza kuwa, kesho watapambana ili kurudisha furaha kwa mashabiki wao.

Kuhusu matokeo mabaya yaliyowaandama siku za karibuni, Kifaru amesema tayari Kocha Mayanga ameshayafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza kwenye michezo hiyo, na amewahakikishia kikosi kitapambana vilivyo kesho Jumamosi.

“Msimu uliopita Young Africans walitufunga hapa, sasa awamu hii hatutaki yajirudie, Kocha Mayanga amesema anahitaji ushindi katika mchezo wetu wa kesho kwa sababu amekiandaa kikosi chake vizuri kwa ajili ya kupambana,”

“Tunakubali matokeo hayajawa rafiki kwetu kwa siku za karibuni, na Kocha wetu amekuwa katika nafasi nzuri ya kurekebisha makosa yaliyojitokeza hadi kupata matokeo mabaya dhidi ya Ihefu FC, na ndio maana amesisitiza maandalizi yamekamilika vizuri tayari kucheza na Young Africans.” amesema Kifaru

Tayari Young Africans imeshawasili mjini Morogoro tangu jana Alhamis (Desemba 28), na wakati wowote itaanza safari ya kuelekea Wilayani Mvomero yalipo maskani ya Mtibwa Sugar.

Video: Upekee wa Rais Samia mwaka 2022
Ripoti: Deni la Taifa linaathiri mapato ya ndani