Kocha Mkuu wa Young Africans Nasreddine Nabi amesema, kazi kubwa iliyo mbele ya kikosi chake kwa sasa ni kuhakikisha wanashinda michezo iliyosalia, ili kutetea Taji la Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu wa pili mfululizo.

Young Africans inandelea kuongoza msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikifikisha alama 59, baada ya kuifunga 2-0 Namungo FC juzi Jumamosi (Februari 04), ikifuatiwa na Simba SC yenye alama 53.

Kocha Nabi amesema inapendeza kuona kikosi chake kinapambana na kupata ushindi, kutokana na dhamira waliojiwekeza ya kutetea Taji msimu huu.

Amesema naamini wakiendelea kushinda michezo iliyosalia, suala la kurejea walioyafanya msimu uliopita litakua rahisi kwa wachezaji wake, hivyo amesisitiza kuwa kila mchezo kwao utakuwa na umuhimu wa kusaka alama tatu.

“Sote tunaona Simba SC inashinda michezo yake, hata sisi tuna ubora wa kushinda michezo yetu, hii nimewaambia wachezaji wangu kwamba hakuna nafasi ya kujiona tumemaliza kazi,”

“Acha washinde michezo yao, lakini nasi tunatakiwa kuendelea kucheza kwa ubora wetu huku tukipata matokeo bora tunayoyataka yatakayotusaidia mwishoni mwa msimu mbele ya wapinzani wetu.” amesema Kocha huyo kutoka nchini Tunisia

Young Africans na Simba SC kila mmoja amebakisha michezo minane hadi kufikia ukingoni mwa msimu huu wa 2022/23, huku zikitarajia kukutana zenyewe mwezi April, Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Watano wafariki kwa homa ya uti wa mgongo, maambukizi 37
Fundi simu anusurika kifo kwa 'kikohozi'