Kocha Mkuu wa Young Africans Nasreddine Nabi, ameweka wazi kuwa, mikakati yake ni kuvuna alama tatu kwenye Mchezo wa Mzunguuko wanne wa Kundi D, Kombe la Shirikisho Barani Afrika dhidi ya AS Real Bamako ya Mali.

Mpambano huo umepangwa kuchezwa Kesho Jumatano (Machi 08), Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam kuanzia saa moja usiku.

Kocha Nabi amesema amekiandaa vizuri kikosi chake kuelekea mpambano huo, ambao wamedhamiria kucheza kwa malengo ya kupata ushindi utakaowaweka kwenye nafasi nzuri ya kutinga Robo Fainali.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Jumanne (Machi 07) jijini Dar es salaam kuhusu maandalizi ya mchezo huo, Kocha huyo kutoka nchini Tunisia amesema hawakufurahishwa na matokeo ya mchezo uliopita, kwani walikaribia kupata alama tatu ugenini, lakini bahati haikuwa kwao.

Amesema kutokana na hali hiyo wamefanya marekebisho ya madhaifu yaliyojitokeza kwenye mchezo huo, hivyo ana matumaini ya kuona matokeo mazuri yakipatikana katika Uwanja wa nyumbani.

“Wachezaji wote hawakukurahishwa na matokeo tuliyoyapata kwenye mchezo wa kwanza ugenini, hasa baada ya wenyeji wetu kupata bao la kusawazisha.”

“Hali hiyo imewaongezea Morari wachezaji wangu kupambana katika mchezo wa kesho Jumatano, ili kuhakikisha tunapata alama tatu, ambazo zitakuwa mtaji mzuri kwenye michezo yetu kabla ya kumaliza Hatua hii ya Makundi.”

“Tumejiandaa vizuri kwa ajili ya mchezo huo dhidi ya Real Bamako, tunafahamu mchezo huu ni muhimu sana kwetu, kwa hiyo tutapambana hadi mwisho ili kupata tunachokihitaji.” amesema Nabi

Endapo Young Africans itashinda mchezo wa kesho Jumatano, itafikisha alama 07 kwenye msimamo wa Kundi D, ambao kwa sasa unaongozwa na US Monastir ya Tunisia yenye alama 07, huku TP Mazembe ikishika nafasi ya tatu kwa kufikisha alama 03 na AS Real Bamako ya Mali yenye alama 02.

CAF yazitamanisha Simba SC, Young Africans
Sarakasi Bungeni imelipa: Massay kujengewa Barabara ya lami