Serikali imeziagiza halmashauri zote nchini kuwafikisha mahakamani na kuuza mali za wadaiwa sugu wa kodi ya pango la ardhi wenye madeni ya muda mrefu na walioshindwa kulipa madeni yao.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Angelina Mabula mara baada ya kufanya ziara ya kukagua mifumo ya makusanyo ya kodi ya ardhi mkoani Geita ambapo amekuta majina 100 ya wadaiwa wa kodi ya ardhi ambao hawajalipa kwa zaidi ya miaka 10.

Amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya mji wa Geita kuhakikisha wadaiwa hao wa muda mrefu wanaandikiwa notisi ya muda wa siku 14 na wasipolipa ndani ya muda huo wafikishwe mahakamani bila kuchelewa na kama wasipolipa basi mali zao zipigwe mnada.

 

Aidha, Naibu Waziri huyo ametembelea eneo lenye viwanja vilivyowekwa mpango wa matumizi bora ya ardhi katika wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita ambavyo vimepangwa kujengwa ofisi za serikali, shule, hospitali, makazi, maeneo ya kuzikia, na huduma nyingine za kijamii.

 

Hata hivyo, Mabulla amezitaka halmashauri nyingine nchini kuiga mfano wa halmashauri ya mji wa Geita kwa kuwashirikisha NHC katika kujenga nyumba bora badala ya kutumia wakandarasi wa nje wakati Shirika la Nyumba la Taifa lipo na linajenga nzuri na kwa gharama nafuu.

 

Video: DC Mjema ateta na wadau wa maji jijini Dar
Mahakama yamfutia shtaka aliyekuwa kiongozi UVCCM