Meneja wa Kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Nadir Haroub ‘Canavaro’ amewatoa hofu Mashabiki wa Soka la Bongo, kwa kutoa taarifa za maendeleo ya Kambi ya timu hiyo inayoendelea jijini Dar es salaam.

Stars ilianza Kambi ya Maandalizi ya mchezo wa Kuwania kufuzu Fainali za Mataifa Bingwa Barani Afrika ‘CHAN 2023’ dhidi ya Uganda juzi Jumatatu (Agosti 22), katika Viwanja vya JK Park jijini Dar es salaam.

Nadir amesema wachezaji wote walifika kwa wakati Kambini na wanaendelea vizuri na Maandalizi chini ya Kocha Kim Poulsen, ambaye amedhamiria kupata ushindi dhidi ya Uganda.

Amesema upande wa wachezaji wote wameonesha kuwa na ari ya kupambana, huku wakisisitiza kucheza kwa uzalendo katika mchezo dhidi ya Uganda ambao utaamua hatma ya Taifa Stars.

“Kila mchezaji ana ari kubwa ya kufanya vizuri, maandalizi yanaendelea vizuri na wachezaji wote walifika Kambini kwa wakati, Kocha anaendele kuwapa mazoezi ya kutosha kuhakikisha tunapata ushindi katika mchezo huo muhimu.” amesema Nadir Haroub

Naye Beki wa kulia Shomari Kapombe amesema wachezaji wote wana morari ya kutosha kuelekea katika mchezo huo, na wanaamini watafuzu kucheza Fainali za CHAN 2023.

Stars itaanzia nyumbani Uwanja wa Benjamin Mkapa Jumamosi (Agosti 27), kabla ya kwenda Uganda kwa mchezo wa Mkondo wa pili ambao utatoa matokeo ya Jumla ili kuamua nani anasonga mbele kwenye Fainali za CHAN 2023 zitakazopigwa nchini Algeria.

Madaktari wathibitisha rasmi uwepo wa Ebola
Afisa Mipango abaka mtoto ndani ya gari, afikishwa Mahakamani