Mabingwa watetezi wa kombe la FA nchini England, klabu ya Arsenal, wamekua wa mwisho kutinga katika hatua ya robo fainali ya michuano hiyo baada ya kufanya vyema katika mchezo wa marudio dhidi ya Hull City ambao ulichezwa usiku wa kuamkia hii leo.
Mchezo huo ulilazimika kurudiwa baada ya ule wa mkondo wa kwanza kumalizika kwa matokeo ya sare ya bila kufungana kwenye uwanja wa Emirates, huko kaskazini mwa jijini London.
Katika mchezo wa usiku wa kuamkia hii leo ambao ulichezwa kwenye uwanja wa KC, Arsenal walichomoza na ushindi wa mabao manne kwa sifuri ambayo yalipachikwa wavuni na washambuliaji Olivier Giroud aliyefunga mawili na Theo Walcott aliyefunga mawili pia.
Kwa mantiki hiyo sasa Arsenal watacheza mchezo wa hatua ya robo fainali mwishoni mwa juma hili dhidi ya Watford, ambao watalazimika kusafiri hadi kaskazini mwa jijini London.
Michezo mingine ya hatua ya robo fainali ya michuano ya kombe la FA itakayochezwa mwishoni mwa juma hili itashuhudia,
Reading v Crystal Palace
Everton v Chelsea
Manchester United v West Ham United