Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, jioni ya leo imetwaa ubingwa wa michuano maalumu iliyomalizika jijini Ndola nchini Zambia baada ya kutoa suluhu dhidi ya Zanaco FC ndani ya Uwanja wa Levy Mwanawasa.

Sare hiyo imeifanya Azam FC kufikisha jumla ya pointi tano sawa na washindi wa pili Zanaco, lakini imewazidi washindi wa pili hao wa Ligi Kuu Zambia, kwa wastani wa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Azam FC kama ingekuwa makini kwenye mchezo huo huenda ingejiandikia bao la kuongoza dakika ya 8 baada ya kufanya shambulizi kali langoni mwa Zanaco.

Lakini shuti alililopiga Kipre Tchetche nje kidogo ya eneo la 18, lilipanguliwa na mlinda mlango na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.

Licha ya juhudi za Zanaco FC nao kutaka kupata bao kwa kufanya mashambulizi kadhaa, safu ya ulinzi ya Azam FC na eneo la kiungo lilikuwa makini kuondoa hatari zote.

Azam FC ilipoteza nafasi nyingine dakika ya 41 baada ya beki Shomari Kapombe kuingia vizuri kwenye eneo la 18 la Zanaco akipokea pande safi la Tchetche, lakini shuti alilopiga lilitoka sm chache ya lango.

Hivyo, hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza kinamalizika timu zote ziliweza kutoshana nguvu kwa kutofungana, ambapo kipindi cha pili kilianza kwa Azam FC kufanya mabadiliko matatu, akitoka beki Pascal Wawa na nafasi yake kuchukuliwa na kiungo Jean Mugiraneza, mwenye uwezo wa kucheza nafasi zote za ulinzi uwanjani kasoro golini.

Wengine waliotoka kwa upande wa Azam FC ni nahodha John Bocco ‘Adebayor’ na kuingia Allan Wanga, pia alitoka Salum Abubakar ‘Sure Boy’ na kuingia Mudathir Yahya, mabadiliko ambayo yalisaidia kuimarisha zaidi eneo la kiungo na Azam FC kumiliki sehemu kubwa ya mchezo.

Dakika ya 72 Allan Wanga alishindwa kutumia vema pasi ya Domayo baada ya kuchelewa kufunga bao akiwa anatazaman na kipa wa Zanaco kufuatia mabeki kumuwahi na kuokoa hatari hiyo, dakika mbili baadaye Azam FF alitoka Thetche na kuingia Ame Ally ‘Zungu’.

Kutokana na Azam FC kuhitaji sare tu au ushindi katika mchezo huo ili kuibuka mabingwa, ilibadilisha mchezo kuelekea dakika 20 za mwisho na kucheza soka la kujilinda zaidi na hadi dakika 90 zinamalizika iliweza kutimiza lengo lake hilo.

Mara baada ya mchezo huo kumalizika timu zote mbili zilipata fursa ya kupongezana pamoja na kusalimiana na waamuzi, kuashiria kutimiza sheria ya kiungwana mchezoni ya ‘Fair Play’.

Wakati Azam FC ikiwa inashiriki kwa mara ya pili michuano hiyo, kihistoria timu ya Power Dynamos ya Zambia ndio timu ya kwanza kutwaa ubingwa huo mwaka juzi kabla ya mwaka jana kuchukuliwa na TP Mazembe, ambayo ilienda kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita.

Azam FC kutwaa ubingwa huo kunaifanya izidi kujiongezea mataji waliyotwaa msimu huu tokea kurejea kwa Kocha Stewart Hall, kufuatia Agosti mwaka jana kutwaa taji la michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA Kagame Cup).

Kikosi cha Azam FC kinatarajia kuanza safari ya kurejea Tanzania kesho usiku na kitawasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl Nyerere (JNIA) Ijumaa Alfajiri.

Kikosi Azam FC;

Aishi Manula, Ramadhan Singano ‘Messi’, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni, Abdallah Kheri, Pascal Wawa/Mugiraneza dk45, Michael Bolou, Frank Domayo, Salum Abubakar/Mudathir dk45, Kipre Tchetche/Ame dk 74, John Bocco (C)/Wanga dk45

Picha: shabiki Yanga Apoteza Fahamu Baada Prisons Kupachika Bao La Pili
Simba Yaendelea Kumkimbiza Mwizi Kimya Kimya