Klabu ya Barcelona imepanga kuishtaki Paris St-Germain (PSG) kwenye taasisi ya kuchunguza masuala ya fedha ya klabu inayohakikisha matumizi ya klabu hayazidi mapato ‘Financial Fair Play investigation’ kufuatia mpango wake wa kumsajili Neymar da Silva Santos Júnior.

Uamuzi huo wa Barca unatokana na kutokubaliana na ubavu wa PSG kutaka kumsajili Neymar kwa 222m euros, kiwango ambacho kitaweka rekodi ya dunia ya usajili.

Ripoti ya Neymar kuwa mbioni kuhamia PSG imewaweka tumbo joto Barcelona ambao licha ya kudai kuwa mchezaji huyo hataondoka wanaona kuna kila dalili za kushindwa kukabiliana na sumaku ya kitita cha fedha kinachomvuta.

Katika mahojiano aliyofanya hivi karibuni na Mundo Reportivo, Rais wa La Liga, Javier Tebas alisema kuwa watachukua hatua za kisheria dhidi ya PSG kama wataendelea na mpango wao wa kutumia kiasi hicho cha fedha ambacho wanaamini hakilingani na mapato yao.

Aliongeza kuwa alikutana uso kwa uso na Rais wa PSG, Nasser Al-Khelaifi na kumueleza ukweli kuwa watachukua hatua hizo dhidi ya klabu hiyo. Alisema Nasser Al-Khelaifi alikasirishwa na kauli yake lakini alibaki akijua ukweli wa kinachoendelea.

“Tutawasilisha malalamiko yetu Uefa na kama hawatachukua hatua yoyote tutayawasilisha kwenye mamlaka za usuluhishi katika ushindani nchini Switzerland na Brussels. Baada ya hapo tunaweza kwenda katika mahakama za Ufaransa na Uhispania,” alisema.

Alisisitiza kuwa wanaamini PSG wamevunja sheria na kanuzi za ‘Financial Fair Play’ pamoja na kanuni za ushindani za umoja wa Ulaya.

Hata hivyo, imeripotiwa kuwa PSG wamepanga kumpa Neymar mkataba wa miaka mitano huku wakidaiwa kuandaa tukio kubwa la mapokezi litakalofunika lile la kumpokea Zlatan Ibrahimovic.

Aliyefunga ndoa na Laptop yake aiburuza serikali mahakamani, Jaji aridhia…
George Weah ajitosa tena Urais wa Liberia