Uongozi wa Mtibwa Sugar umetangaza vita ya kufa na kupona katika michezo miwili ya mwisho ya Ligi Kuu Tanzania Bara, ili kupambania kubaki kwenye ligi hiyo kwa msimu ujao 2022/23.

Mtibwa Sugar ipo nafasi ya 12 kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na alama 31, ambazo hazitoshi kuihakikishia kubaki Ligi Kuu kwa msimu ujao, hivyo inahitaji alama sita za michezo miwili.

Mabingwa hao wa Tanzania Bara mara mbili mfululizo msimu wa 1998/99 na 1999/2000, watapambana na Namungo FC nyumbani Manungo Complex mkoani Morogoro, kabla ya kurejea jijini Dar es salaam kumalizana na Young Africans kwenye mchezo wa mwisho utakaopigwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasilino ya klabu hiyo Thobias Kifaru amesema bado kikosi chao kina nafasi ya kuendelea kupambana ili kubali Ligi Kuu msimu ujao, hivyo wanatangaza rasmi Vita ya Kufa na Kupona dhidi ya Namungo FC na Young Africans.

“Bado tuna michezo miwili imesalia, tuna nafasi ya kuendelea kuwa sehemu ya timu za Ligi Kuu msimu ujao, tutahakikisha tunajipanga vizuri na kumaliza kwenye nafasi ambayo tutakuwa salama,”

“Tunarudi nyumbani kwa ajili ya kucheza na Namungo FC, kisha tutarudi hapa Dar es salaam kucheza na Young Africans katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, kwa hiyo tutapambana hadi mwisho ili kuishinda hii vita,” “Lolote linaweza kutokea katika hii michezo miwili, nina uhakika Mtibwa haitashuka daraja kwa sababu tuna uzoefu wa kutosha wa kupambana katika hali kama hii, hiki ni chuo tunajua namna ya kutumia karata zetu.”amesema Kifaru

Balozi Mulamula akataa migogoro ya Jumuia ya Madola
Bunduki kuanza kudhibitiwa Marekani