Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo ameliomba Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO), kuendelea Kuunga mkono mipango ya Serikali ya Tanzania katika usimamizi wa mazingira na kupambana na athari za mabadilko ya Tabianchi bna kuliomba shirika hilo kuisaidia Tanzania kitekenolojia, ubunifu, mafunzo na masuala ya kifedha kwa miradi ya maendeleo, katika Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi hususan Ajenda 10/30.

Jafo metoa ombi hilo alipokutana na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa FAO, Maria Helena Semedo katika Mkutano wa Uwili jijini Nairobi nchini Kenya wakati wa Mkutano wa Sita wa Baraza wa Mazingira Duniani (UNEA6).

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Selemani Jafo akizungumza na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) Bi. Maria Helena Semedo (hayupo pichani) katika Mkutano wa Uwili wakati wa Mkutano wa Sita wa Baraza wa Mazingira Duniani (UNEA6) jijini Nairobi nchini Kenya. Kulia ni Afisa Mazingira Mwandamizi Ofisi ya Makamu wa Rais, Simeon Shimbe.

Katika kikao hicho kilicholenga kuimarisha uhusiano baina ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na FAO, Dkt. Jafo amelishukuru kwa kazi kubwa
wanayofanya nchini tangu Tanzania ijiunge na shirikia hilo mwaka 1962 na tangu shirika hilo lilipofungua Ofisi zake nchini mwaka 1977.

Amesema, FAO imekuwa ikishirikiana vyema na Tanzania katika kujengea uwezo wataalamu wa Serikali, kusaidia katika usalama wa chakula sambamba na sekta ya Kilimo, Mazingira na masuala mbalimbali ya kimaendeleo.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Selemani Jafo (wa tatu kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) Bi. Maria Helena Semedo (katikati) mara baada ya Mkutano wa Uwili wakati wa Mkutano wa Sita wa Baraza wa Mazingira Duniani (UNEA6) jijini Nairobi nchini Kenya.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mkuu Bi. Semedo amemuhakikisha Waziri Dkt. Jafo na Serikali ya Tanzania kwamba FAO itaendelea kudumisha ushirikiano wao kwa kuweka nguvu katika sekta ya Mazingira na ameihakikishia Tanzania kuwa shirika litaendeleza utekelezaji wa
mipango mbalimbali ya maendeleo hususan kuongeza tija katika kilimo, ili Tanzania iweze kufikia malengo iliyojiwekea.

Mkutano huo, uliofanyika Februari 26 hadi Machi 1, 2024 ulichagizwa na kaulimbiu isemayo “Juhudi Madhubuti, Jumuishi na Endelevu
za Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Uharibifu wa Bioanuai na Uchafuzi” na ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Waziri Dkt. Jafo akiambatana na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdallah Hassan Mitawi pamoja na wataalamu kutoka Ofisi hiyo.

Vijana wahimizwa kushiriki shughuli za kimaendeleo
Dkt. Msonde aagiza utolewaji mafunzo mfumo wa NeST