Rais wa Shirikisho la Soka nchini Tanzania ‘TFF’, Wallace Karia amesema kuna asilimia kubwa nchi za Afrika Mashariki (Tanzania, Kenya na Uganda) zikaandaa fainali za mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani ‘CHAN 2024’ baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa na Shirikisho la Soka Barani Afrika ‘CAF’.

Amesema kuwa huenda nchi hizo zikapata nafasi hiyo baada ya kuwa ndio nchi pekee zilizoomba nafasi hiyo ya kuwa wenyeji hadi sasa. Michuano inayotarajia kufanyika kati ya Septemba na Oktoba mwaka huu.

“Rais Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na Marais wa Kenya William Ruto na Yoweri Museveni wa Uganda wamezungumza na Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika ‘CAF’, Patrice Motsepe hivyo tunaweza tukaandaa fainali za mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani ‘CHAN 2024’.

“Kwa asilimia kubwa wamekagua miundombinu na wametuelekeza baadhi ya vitu tuvirekebishe, tulirekebisha na wameridhishwa na uboreshwaji huo,” amesema.

Ameongeza kuwa shida iliyopo ni viwanja vya mazoezi lakini katika kuhakikisha hilo wanalifanyia kazi wamezungumza na Wizara kupitia kurugenzi ya michezo kuna viwanja viwili vitarekebishwa hapa Dar es salaam na Zanzibar tayari vipo viwili.

“Wakati tunaomba kuandaa ‘AFCON 2027’ kulikuwa na upinzani sana, jambo moja tulilosema tukipata tunaweza kuwa wenyeji wa ‘CHAN 2024’ ikiwa kama matayarisho ya fainali za mataifa ya Afrika.

Tunasubiri kutangazwa kwa tarehe, nadhani Aprili Mosi, kikao cha kamati ya utendaji ya ‘CAF’ inawezekana tukapitisha hiyo kuwa sisi tukawa wenyeji wa mashindano haya,” ameongeza

Majaliwa: Mawakili, Maafisa Sheria wazingatie weledi
Utoaji Leseni Madini ya Metali kusaidia ukuzaji wa uchumi