Mchezaji na kinda wa Mabingwa wapya wa barani Ulaya (Euro 2016) Renato Sanches ametajwa kuwa mchezaji bora kijana wa fainali za barani humo ambazo zilifikia tamati  usiku wa kuamkia hii leo jijini Paris nchini Ufaransa.

Kiungo huyo mwenye uwezo wa hali ya juu, ameshinda tuzo hiyo na kuwashinda wenzake Kingsley Coman wa Ufaransa na Mreno mwenzie Raphael Guerreiro.

Zawadi hizo ambazo zilikuwa maalum kwa wale wote waliozaliwa baada ya January mosi mwaka 1994, zilitolewa na jopo la wataalamu wa masuala ya kiufundi wa UEFA lililokuwa likiongozwa na Lupescu.

Wengine waliokuwa kwenye jopo hilo ni Sir Alex Ferguson na Alain Giresse.

Sanches alianza kuonesha uwezo wake pale tu alipopewa nafasi kwenye mchezo dhidi ya Poland na kuonesha kiwango bora kabisa kilichomshawishi kocha wake kumuanzisha kwenye mechi zilizofuata.

Sanches alifunga goli lake la kwanza kwa timu yake katika mchezo dhidi ya Poland na kumfanya kuwa mchezaji wa tatu kijana kucheza mchezo wa fainali ya Euro mwaka huu.

Alikuwepo kwenye michezo yote muhimu ambayo Ureno walipata ushindi, ambayo ni dhidi ya Wales ambapo walishinda 2-0 na jana dhidi ya Ufaransa na kumfanya kushinda tuzo hiyo katika umri mdogo zaidi wa miaka 18 na siku 328.

Kinda huyo mzaliwa wa Lisbon, ambaye kwenye dirisha hili la usajili amejiunga na FC Bayern München akitokea Benfica kwa ada ya awali ya uero milioni 35, alianza msimu wa 2015/16 akiwa na timu B ya Benfica na kushiriki katika Michuano ya Ligi ya Vijana ya UEFA, Michezo ya kufuzu Michuano ya Ulaya kwa vijana chini ya miaka 19 na vile vile Ligi ya Mabingwa Ulaya kabla ya kupata nafasi ya kucheza timu ya taifa ya Ureno kwa mara ya kwanza Machi 25 mwaka huu.

Renato Sanches na Kingsley Coman msimu ujao watakuwa wote kwenye klabu ya Bayern huku Raphael Guerreiro naye atakuwa nchini Ujerumani lakini akikipiga kunako klabu ya Borussia Dortmund.

Antoine Griezmann: Sina Furaha Na Tuzo Ya Ufungaji Bora
Aldridge: Paul Pogba Hana Thamani Ya Pauni Milion 100