Beki wa kushoto wa Simba, Gadiel Michael anatakiwa katika viunga vya Chamazi kwa kupewa nafasi ya kurejea kwenye timu hiyo kwa ajili ya msimu ujao.

Mkataba wa Gadiel ndani ya Simba unamalizika Mwishoni mwa msimu huu na hayupo katika sehemu ya wachezaji watakaoongezewa mkataba.

Beki huyo alitokea katika akademi ya Azam FC na kucheza timu ya wakubwa kabla ya msimu wa 2014/15 kuondoka na kujiunga Young Africans.

Habari kutoka kwa mtu wa karibu na Gadiel Michael zinaeleza kuwa uongozi wa Azam FC unaushawishi mkubwa kwa mchezaji huyo, na huenda akawa sehemu ya watakaosajiliwa klabuni hapo mwishoni mwa msimu huu.

Mabosi wa Azam FC nao kwa sasa wapo kwenye mipango ya kuachana na beki wao wa kushoto, Bruce Kangwa na jambo hilo linampa nafasi Gadiel.

Awali, Gadiel alikuwa anatajwa kujiunga na Singida Big Stars, lakini dili hilo limeonekana kuwa gumu baada ya kusajiliwa kwa Yahya Mbegu.

Chanzo kimoja kilicho karibu na mchezaji huyo kimedokeza kuwa: “Gadiel anataka acheze tena mashindano ya kimataifa na ndiyo maana watu wake wapo kwenye mazungumzo na Azam FC.”

Alipotafutwa msemaji wa Azam FC, Hasheem Ibwe kuzungumzia uwezekano huo, alisema kwa kifupi: “Azam FC itafanya usajili ili timu iwe bora zaidi na kuleta ushindani, lakini siwezi kusema ni wangapi wanaingia.”

Kwenye kikosi cha Simba, Gadiel hajawa na wakati mzuri baada ya kukosa nafasi ya kucheza mbele ya Mohamed Hussein ‘Tshabalala’.

Ndani ya miaka minne akiwa na Simba, beki huyo hajawa chaguo la kwanza, jambo ambalo linawalazimu mabosi wa Simba kutafuta mchezaji mwingine kwenye eneo hilo.

Serikali kuwekeza bilioni 2.2 kukiendeleza kilimo cha mirungi
Feisal apitishwa usajili wa Simba SC 2023/24