Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema serikali imekusudia kutoa bima za afya kwa wote kwa watanzania milioni 4.5 sawa na asilimia 30 ya watu milioni 15 ambao ambao hawana uwezo wa kugharamia huduma za afya.

Utaratibu wa bima hiyo hautaanza kwa watu wote bali kwa waliopo katika ajira za sekta binafsi na makundi maalumu.

Ummy amesema hayo Dodoma wakati wa semina ya kuwajengea uwezo wabunge kuhusu muswada wa bima ya afya kwa wote.

Amesema kwa sasa Watanzania wasiojiweza ni takribani milioni 15 na kuwa mpango wa awali ni kuanza kuhudumia asilimia 30 ya kundi hilo ambao ni sawa na watu milioni 4.5 na watapatikana kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (TASAF).

“Hatutaanza kwa Watanzania wote kuingia kwenye mfuko, bali tutaanza na walio na sekta rasmi na baadaye tutayajumuisha makundi mengine hatua kwa hatua,” amesema Ummy.

“Kwa Watanzania wasio na uwezo wa kulipia tutaanza takwimu zinazoonesha tuna wananachi milioni 15 hivyo sasa tutaanza kwanza na asilimia 30 ya miaka 25 ya Watanzania na njia tuliyotumia kuwapata ni kutumia Tasaf.”

Aidha Ummy amesema gharama zilizopendekezwa zimefanyiwa utafiti wa kina na kuonekana wananchi wengi watazimudu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote bila kubagua.

Hata hivyo amesema chanzo cha kupata fedha ili kugharamia matibabu kwa watu wasiokuwa na uwezo, watashauri zitozwe kwenye bia, juisi, kumbi za starehe pamoja na maeneo mengine kadri watakavyoona.

Mhandisi Chiwelesa: TANROADS isipewe miradi ya ujenzi viwanja vya ndege
Hersi Said: Wapuuzeni wasioitakia mema Young Africans