Siku moja baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) kutangaza donge nono la shilingi Milioni 10 kwa atakayefanikisha kukamatwa kwa aliyekuwa Mhasibu wa Taasisi hiyo, Godfrey Gugai kwa tuhuma za kujipatia mali nyingi kinyume na sheria ya Utumishi wa umma, ameibuka na kusema kuwa hajatoroka na kwamba yupo nchini.

Mhasibu huyo, Godfrey Gugai amesema kuwa taarifa zilizotangazwa za kuwa anatafutwa zimemsikitisha kwani yeye yupo nchini na hajatoroka kwenda mahala popote, hivyo yuko tayari kuendelea kutoa ushirikiano.

“Nimesikitika kwa sababu kwa taasisi kama TAKUKURU, taasisi yenye dhamana ya uchunguzi, sikutegemea kiongozi mwenye dhamana aseme kwamba nimekimbilia Congo, kwa sababu taasisi kama hiyo yenye dhamana ilikuwa na wajibu wakuangalia kwenye mipaka kama kweli nimekwenda nje ya nchi,”amesema Gugai

Aidha, kuhusu tuhuma zilizotolewa dhidi yake amesema kuwa ameamua kufika makao makuu ya TAKUKURU ili kusudi suala hilo liweze kwenda Mahakamani kwa sababu mahakama ndio chombo pekee chenye kutoa haki.

Hata hivyo, kufuatia donge nono lililotangazwa siku ya tarehe 14 Nov 2017 na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Brigedia Jenerali John Mbung’o kuwa atakaye fanikisha kukamatwa kwa mhasibu huyo, Godfrey Gugai atapewa Milioni 10, mhasibu huyo amesema kuwa, Rais wa Tanzania ana mapambano ya kuminya matumizi ili kuleta huduma bora za afya kwa wananchini hivyo fedha hizo zipelekwe hospitalini zikasaidie kutoa huduma kwa jamii.

Vilevile ametahadharisha asije akajitokeza mtu yeyote atakayedai kafanikisha kupatikana kwake ili ajipatie fedha hizo, kwani yeye alikuwepo na amejitokeza mwenyewe na hakuna mtu aliyemfuata.

Video: Makonda aahidi kutatua changamoto za mabaharia
JPM aagiza kubomolewa kwa Jengo la Tanesco Ubungo