Licha ya kufanya vizuri katika michezo ya Hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika msimu huu 2022/23, Kocha Mkuu wa Al Hilal ya nchini Sudan, Florent Ibenge amedhamiria kukiboresha maradufu kikosi chake kwa msimu ujao wa 2023/24.

Ibenge alijiunga na Al Hilal mwanzoni mwa msimu huu, baada ya kuiwezesha RS Berkane ya Morocco kutwaa Ubingwa wa Kombe la Shirikisho Barani Afrika msimu uliopita 2021/22, kwa kuifunga Orlando Pirates ya Afrika Kusini.

Kocha huyo kutoka DR Congo ameanza ushawishi kwa uongozi wa Al Hilal ili kuipata saini ya Beki tegemeo wa Simba SC, Hennock Inonga Baka raia wa DR Congo.

Mipango ya Kocha huyo kumpendeka Inonga ni kuhakikisha anakiboresha kikosi chake kwa kuanzia safu ya ulinzi ya timu hiyo, ambayo ameona inahitaji kuboreshwa zaidi.

Inonga ni kati ya wachezaji tegemeo katika kikosi cha Simba SC, ambaye msimu huu aliongezwa mkataba mwigine wa miaka miwili na sasa anatakiwa na kocha huyo ambaye pia ana uraia wa DR Congo.

Taarifa kutoka jijini Dar es salaam zinaeleza kuwa, uongozi wa Simba SC haupo tayari kumwachia Inonga ambaye mwishoni mwaka 2022 alisaini mkataba mpya hadi mwaka 2025.

Mtoa taarifa hizo amesema kuwa kama uongozi utakubali kumuachia beki huyo basi watalazimika kuununua mkataba wa miaka miwili Simba ambao ameubakisha.

Aliongeza kuwa beki mwenyewe yupo tayari kuondoka klabuni hapo kama atawekewa maslahi mazuri mezani.

“Kocha wa Al Hilal, Ibenge anaangalia uwezekano wa kumsajili Inonga katika dirisha kubwa la usajili mwishoni mwa msimu huu.

“Hivyo Al Hilal watatakiwa kununua sehemu ya mkataba wake ambao ameubakisha wa miaka miwili aliokuwa nao Simba, kama kweli wanamuitaji Inonga kwa ajili ya msimu ujao.

“Ibenge amepanga kukiboresha kikosi chao kwa kuanzia safu ya ulinzi ambayo kwake ameiona ndio inahitaji maboresho makubwa,” amesema mtoa taarifa huyo.

Hata hivyo Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba SC Ahmed Ally amesema: “Kama uongozi hatumzuii mchezaji yeyote kuondoka hapa Simba, kikubwa taratibu zifuatwe za usajili.”

Chris Sutton amkataa Bruno Fernandes Man Utd
Makala: Siri ya Mwanamke kujikomboa