Shirika la Fedha Duniani (IMF) limeahidi kuipatia Tanzania fedha itakayoihitaji ili iweze kuendelea kukabiliana na athari zitokanazo na janga la Covid 19 kwa ajili ya kuimarisha uchumi wake.

Mkurugenzi Mkazi wa IMF nchini Tanzania Jens Reinke ameyasema hayo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamamba John Kabudi katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam.

Reinke ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua madhubuti inazozichukua  katika kukabiliana na janga la Covid 19 ili kuepusha madhara ya kiuchumi na kijamii.

Mazungumzo hayo pia yamelenga miradi ya maendeleo, msamaha wa madeni kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania, ushirikiano baina ya IFM na Tanzania, biasara na utalii.   

Kwa upande wake, Prof. Kabudi ameishukuru (IMF) kwa msamaha wa madeni ambao umetolewa kwa Tanzania na nchi nyingine, fedha zitakazoziwezesha nchi hizo kuendelea kukabiliana na Covid 19.

“Tumeongelea mambo mbalimbali yanayohusu ushirikiano hasa katika kuimarisha uchumi wetu baada ya janga la covid 19, usirikiano kati ya Tanzania na IMF unafahamika na tumekubaliana baadhi ya mambo ambayo tutayafanyia kazi kwa kina ili tuweze kuimarisha uchumi wetu baada ya corona hasa katika sekta ya utalii, biashara na miundombinu,” amesema Prof. Kabudi.

Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi amekutana na kumuaga Balozi wa Vietnam nchini, Mhe. Nguyen Kim Doanh ambaye amemaliza muda wake wa utumishi na amemtakia maisha mema na kumsihi kuendelea kuwa balozi mwema kwa Tanzania nchini Vietnam na duniani kwa ujumla.

“Kwa niaba ya Serikali napenda kukuhakikishia kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Vietnam katika nyanja mbalimbali za kimataifa ikiwemo kuiunga mkono Vietnum katika kugombea nafasi mbalimbali katika Masirika ya KImataifa,” Amesema Prof. Kabudi

Nae Balozi Doanh ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikimpatia alipokuwa akitekeleza majukumu yake nchini wakati wote na kuahidi kuwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili utaendelea kuimarishwa.

Zimbabwe yasitisha miamala ya fedha kwa simu
Rais Mutharika ataka matokeo ya awali kupuuzwa