Wananchi wa Mkoa wa Dar es salaam wameombwa kuhudhuria kwa wingi katika maadhimisho ya siku ya kumbukumbu ya mashujaa julai 25 ambayo kimkoa yanatarajiwa kufanyika katika viwanja vya mnazi mmoja huku Kitaifa yakitarajiwa kuwa mkoani Dodoma.
Leo wakati akitoa taarifa kwa wanahabari Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mh. Paul Makonda amesema maadhimisho hayo ni muhimu kwa nchi kwani yanajenga kuwaenzi wale waliojitolea kupambana kwa ajili ya kulinda amani, na utulivu katika nchi.
Aidha katika maadhimisho hayo matukio mbalimbali yanatarajiwa kuchukua nafasi kama uwekaji wa silaha za asili na maua kwenye minara wa kumbukumbu huku matukio hayo yakiongozwa na sala kutoka kwa viongozi mbalimbali wa dini hapa nchini.
Pamoja na hayo Mh. Makonda amesisitiza usafi katika maeneo yote ya jiji la Dar es salaam hasa katika maeneo yanayozunguka viwanja vya mnazi mmoja.
Maadhimisho haya ya kuwakumbuka Mashujaa yatafanyika jumatatu ya julai 25 kuanzia saa mbili asubuhi mpaka saa 6 mchana huku Mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Mh. Paul Makonda.