Serikali imetangaza rasmi kuanza kutumika kwa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumsihi wa Umma (PSSSF) kuanzia Agosti 1, mwaka huu.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, ambapo amesema kuwa Serikali imekamilisha maandalizi yote muhimu ya utekelezaji wa Sheria ya PSSSF na imeridhika kwamba Mfuko huo unaweza kuanza kutekeleza majukumu yake.

“Napenda kutangaza rasmi kwamba, kwa mamlaka niliyonayo chini ya kifungu cha 1(1) cha Sheria ya PSSSF nimeteua tarehe 1 Agosti, 2018 kuwa ndiyo tarehe rasmi ya kuanza kutumika kwa Sheria ya PSSSF,” amesema Mhagama

Aidha, Mhagama amefafanua kuwa, kutokana na hatua hiyo wafanyakazi wote watakaoajiriwa katika sekta ya umma watasajiliwa katika Mfuko wa PSSSF na wale watakaoajiriwa katika sekta binafsi watasajiliwa katika Mfuko wa NSSF.

Hata hivyo, ameongeza kuwa Wanachama wote ikiwa ni pamoja na wastaafu na warithi waliopo katika mifuko inayounganishwa watahamishiwa katika mfuko wa PSSSF na haki na stahili zao zitaendelea kutolewa na mfuko huo bila kuathiriwa kwa namna yeyote ile.

 

Olympic Marseille yajitosa kwa Olivier Giroud
Video: Kangi Lugola amtaka Zitto Kabwe ajisalimishe