Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amekutana na kufanya mazungumzo na wadau wa zabibu kwa lengo la kujadili fursa na changamoto zinazokabili zao hilo ili kulipatia ufumbuzi, katika
ukumbi wa Jakaya Mrisho Kikwete jijini Dodoma.

Senyamule amekutana na katika mazungumzo hayo na kuwataka washiriki wa kikao hicho kuhakikisha wanashirikiana vizuri ili kuweza kuleta Maendeleo ya ndani ya Mkoa na taifa kwa ujumla.

Amesema, “ushirika ndio matumaini makubwa katika kutupa nguvu ya pamoja na kuweza  kukua katika kilimo, nendeni mkasimamie na kutekeleza kwa makini maazimio tuliyokubaliana kwa kuwa tukishirikiana tutafika mbali.”

Aidha, Senyamule amewataka wakulima wa zao hilo kutumia utalaamu wa kisasa ili kuendana na mazingira ya sasa na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu, na kusisitiza matumizi ya mbolea katika kuimarisha upatikanaji wa mazao.

Pia amewasisitiza kuongeza tija katika uzalishaji. Senyamule pia ameipongeza Kampuni ya Jambo Food Products kwa kazi nzuri wanayofanya ya uchakataji wa zao hilo na ameahidi kuwapa eneo kwa ajili ya kuanza Ujenzi wa Kiwanda Mkoani Dodoma.

Kikao hicho, kiliwahusisha wakulima na wanunuzi wa zao hilo na kuhudhuriwa na Anthony Mavunde Naibu Waziri Wizara ya Kilimo, Deogratius  Ndejembi Naibu Waziri Ofisi ya Rais ,Tawala za Mkoa na Serikali za Mtaa (TAMISEMI), Kenneth Ernest Nollo Mbunge wa Jimbo la Bahi, Ally Gugu Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma, Wakuu wa Wilaya tatu Chamwino, Bahi na Dodoma Mjini. 

Idadi watu walionyongwa yazidi kupaa
Mahitaji ya Wakimbizi nchini Sudan ni dola bilioni 3