Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), imethibitisha kutokea kwa tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa kiwango cha 4.7 lilotokea februari 8, 2023, umbali wa kilomita 33 kutoka visiwani Pemba na kusikika katika baadhi ya miji nchi ya Tanzania na Kenya.

Mjiolojia mwandamizi kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Gabriel Mbugoni amethibitisha kutokea kwa tetemeko hilo, na kudai kuwa bado wanaendelea kufuatilia iwapo kuna madhara yametokea.

Amesema, “Ni kweli tetemeko limetokea lenye ukubwa wa kipimo cha 4.7. mpaka sasa bado hatujapata taarifa bado tunaendelea kufuatilia. Tetemeko hili limesikika Pemba, Tanga kwa hapa Tanzania na maeneo mengine jirani mara zote kuna kuwa na chanzo ambacho ni kimoja pekee lakini limekwenda mpaka Kenya.”

Tetemeko hilo, lililotokea katika Bahari ya Hindi limekuja ikiwa ni ikiwa ni siku mbili tangu tetemeko la ardhi la kipimo cha 7.8 kuathiri nchini Uturuki ambapo maelfu ya watu wamepoteza maisha yao na kujeruhiwa na majengo na miundombinu kadhaa kuharibiwa.

Mawimbi ya tetemeko hilo yamedaiwa kusikika jana Februari 8 majira ya saa 12:30 jioni, huku baadhi ya wakazi wa jiji la Tanga nao wakieleza kuwa walilihisi tetemeko hilo.

Bungeni: Muswada Bima ya afya wakwama tena
Udanganyifu hauna namna ya kuutetea: Spika Dkt. Tulia