Tanzania itafikia lengo la kuwa na uhakika wa usalama wa chakula kwa kusimamia sera na miongozo ya uzalishaji wa mbegu bora zitakazotosheleza mahitaji ya ndani na kuondokana na dhana ya utegemezi wa kuagiza pembejeo za kilimo nje ya nchi.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Makongoro Nyerere jijini Arusha wakati wa ufunguzi wa kongamano la wadau wa mbegu waliokutana kujadili ufanisi wa ushirikiano na serikali kwenye kuboresha mazingira ya kisera na udhibiti wa sekta ya mbegu.

Amesema, sera na miongozo ya nchi katika sekta ya kilimo hasa mbegu inatakiwa isimamiwe kikamilifu ili kuwa na mbegu itakayotoa mazao bora yatakayokuza pato la mkulima na kuinua uchumi wa nchi.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara Makongoro Nyerere akikata utepe wa kuzindua mpango mkakati wa mbegu bora.

‘’Wakati ni sasa wa wazalishaji wa mbegu kujikita kutengeneza mbegu bora ili jamii na nchi za jirani ziweze kujua kuwa mbegu bora zipo Tanzania,’’ amebainisha Mkuu huyo wa Mkoa.

Amesema, suala la kilimo halihitaji siasa ili kuwezesha kilimo kuwa cha kibiashara, kunufaisha jamii ya watanzania na wakulima wanaopambana kuhakikisha wanapata mazao bora yatakayowaletea faida na kuinuka kiuchumi.

Naye, Afisa Mtendaji Mkuu Mpango wa Kukuza Kilimo Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT), Geofrey Kirenga amezungumzia muelekeo wa Tanzania kwenye sekta ya mbegu, kwa kusema kuwa kutekeleza dhana ya ushirikishwaji nchini ni moja ya ya mfano wa kuigwa.

Wadau katika kongamano waksikiliza majadiliano kuhusu mbegu bora.

Amesema, wakulima wasipotunza udongo kwa uhakika kupata mbegu bora haitasaidia kufikia malengo kwani wakulima wanapaswa kupata elimu kutoka kwa maafisa ugani ishara ambayo inahitaji utendaji kazi wa pamoja.

Ulemo-Misigiri mbioni kuoga Maji ya RUWASA
Uviko-19 yavuruga utoaji chanjo kwa Watoto