Aliyekua mshambuliaji wa timu ya taifa ya Ufaransa Youri Djorkaeff amemtahadharisha kinda wa AS Monaco Kylian Mbappe, kuhusu mipango ya usajili ambayo inaendelea kusukwa dhidi yake na baadhi ya klabu za soka barani Ulaya.

Djorkaeff amempa tahadhari hiyo Mbappe kwa kutumia mfano wa mshambuliaji mwenzake Anthony Martial, ambaye alisajiliwa na Manchester United akitokea AS Monaco misimu mitatu iliyopita.

Djorkaeff amesema kuna haja kwa Mbappe kufikiria mara mbili kuhusu mipango wa usajili inayoandaliwa dhidi yake kuelekea majira ya kiangazi, ili kutambua mustakabli wa kuendeleza kipaji cha soka alichonacho kwa sasa.

Amesema anaogopa kuona mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 21 akipoteza thamani ya kuendelea kutambulika kama mchezaji mwenye uwezo, hivyo hana budi kukaa chini na watu wake wa karibu na kumpa ushauri wa nini cha kufanya.

Djorkaeff ambaye aliwahi kucheza soka nchini England akiwa na klabu za Bolton Wanderers na Blackburn Rovers, amesema wakati Martial alipojiunga na Man Utd Septemba 2015 kwa ada ya usajili ya Pauni milioni 36, alikua anasifika nchini Ufaransa kwa soka safi na upachikaji mabao, lakini alipofika England sifa zake zilianza kupungua siku hadi siku.

Mbappe anatajwa kuwa kwenye rada za klabu za nchini England na Hispania, lakini mpaka sasa hakuna taarifa yoyote iliyotolewa na uongozi wa AS Monaco kuhusu mustakabali wake baada ya msimu huu kufikia kikomo mwezi Mei.

Mandari atoa elimu kwa wananchi, Ni kuhusu mikopo fedha za ujenzi (Mortgage Finance)
Wizara yawahakikishia umeme wa uhakika wananchi