Kiungo Mshambuliaji kutoka nchini Ghana Augustine Okrah ametoa kauli nzito kuelekea Msimu ujao wa Ligi Kuu, Kombe la Shirikisho ‘ASFC’ na Michuano ya Kimataifa inayoratibiwa na Shirikisho la Soka Barani Afrika ‘CAF’.

Kiungo huyo aliyesajiliwa Simba SC akitokea Bechem United ya nchini kwao, ametoa kauli hiyo akiwa Ismailia-Misri, ambako Kikosi cha Msimbazi kimeweka kambi kwa zaidi ya majuma mawili sasa.

Okrah, ambaye ameeleza kufurahia kusajiliwa na miamba hiyo ya soka nchini amesema amedhamiria kufanya makubwa kuliko aliyoyafanya alikotoka, ambako uwezo wake ulimfanya aitwe kwenye timu ya taifa ya nchi hiyo.

Amesema Simba ilipomfuata alikuwa na dili la Azam FC ya Tanzania pia lakini yeye na wakala wake walibadili uamuzi na kutua Simba.

“Simba ni timu ya ndoto zangu, hapo awali nilikuwa natamani kucheza klabu kubwa kama hii niliyopo sasa, nimefurahi kuwa hapa na kazi iliyobaki ni mimi kuipambania klabu,” alisema Okrah na kuongeza;

“Kilicho mbele yangu ndani ya hii miaka miwili nitakayokuwa Simba ni kuhakikisha napambana na kufanya yaliyo bora zaidi ya kile nilichokuwa nakifanya katika Ligi Kuu ya Ghana.

“Ili kuonyesha Simba hawakukosea kufanya usajili wangu nitapambana ili kupenya katika kikosi cha kwanza na kutoa msaada kwa timu kwa maana ya kuonyesha kiwango bora ikiwemo kufunga mabao mengi, kutoa asisti za mabao na ushirikiano wa kutosha kwa wachezaji wenzangu.

“Unajua Simba ni klabu kubwa na kila mchezaji aliyepo anatakiwa kuipigania na kulinda ukubwa wake, hilo ndio nimeliweka katika moyo wangu pamoja na malengo mengine ambayo naamini nitaenda kuyatimiza.

“Jambo jingine nimefurahishwa na mashabiki wa Simba vile ambavyo wamenipokea kwa heshima kubwa huku wakionyesha wananipenda na wanategemea makubwa kutoka kwangu, naamini nitawafurahisha.” amesema Okrah

Kocha Nabi aitolea uvivu Bodi ya Ligi, TFF
Mtibwa Sugar yatema wachezaji 20, yapandisha vijana