Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kuwa Serikali ya mkoa huo imepanga kuendesha kampeni maalum itakayowezesha ujenzi wa nyumba bora za walimu katika jitihada za kuboresha sekta hiyo.

Akizungumza leo katika ukumbi wa mikutano Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam, Makonda amesema kuwa kampeni hiyo maalum itawezesha ujenzi wa nyumba za walimu 402 zenye kiwango bora cha nyumba za kisasa.

Alisema Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limejitolea kujenga nyumba hizo na kinachotakiwa ni kuwapa vifaa vya ujenzi.

“Haiwezekani walimu wetu wanaowafundisha wanafunzi wetu kupata matatizo ya makazi au hata sehemu za kujistili wawapo katika mazingira ya kazi. Tutawajengea nyumba 402 zenye sehemu za kujistili ndani (self-contained),” alisema Makonda.

Mkuu huyo wa mkoa alitoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam ambao wamekuwa wakiunga mkono kampeni za kuboresha elimu, akiwataka kujiandaa kushiriki kampeni hiyo ili kuwezesha kufikia malengo ya ujenzi wa nyumba hizo.

Awali, mkoa huo ulifikia malengo ya kuondoa tatizo la upungufu wa madawati mashuleni kupitia kampeni maalum ya kuchangia madawati ilyoongozwa na Mkuu huyo wa Mkoa.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam anaendelea na kongamano la kuboresha barabara za mkoa huo, ambapo amekutana na wataalam wa barabara pamoja na bodi ya barabara.

Polisi Dar waanza msako mkali dhidi ya watuhumiwa wa mauaji
Kagame: Afrika inatakiwa kujiongoza yenyewe