Kiongozi wa muungano wa vyama vya upinzani nchini Kenya (NASA), Raila Odinga, ametangaza maandamano ya nchi nzima tarehe iliyopangwa kufanyika uchaguzi wa marudio nchini humo, ambao unatarajiwa kufanyika tarehe 26 Oktoba mwaka huu.

Akizungumza wakati akiwahutubia wafuasi wake katika mtaa wa Kamukunji jijini Nairobi, amesema kuwa ataendelea kushinikiza marekebisho katika tume ya uchaguzi ili kuweza kufanyika uchaguzi wa haki.

“Leo tunabadilisha kauli mbiu yetu kutoka hakuna mabadiliko hakuna uchaguzi, sasa ni hakuna uchaguzi Oktoba 26,”amesema  Odinga huku akisisitiza kuwa amejiondoa kutoka kwenye mchakato wa uchaguzi huo.

Aidha, Odinga ametoa kauli hiyo mara baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuonya kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote ambaye atajaribu kuvuruga marudio ya uchaguzi huo tarehe 26 Oktoba mwaka huu.

Hata hivyo, haya yanajiri mara baada ya moja wa maafisa wakuu wa Tume ya Uchaguzi Kenya (IEBC) Dkt. Roselyn Akombe kutangaza kujiuzulu katika tume hiyo chini ya wiki moja kabla ya uchaguzi mpya wa urais kufanyika nchini humo.

Video: Mungu alisema sitakufa - Tundu Lissu, Serikali yalipa madeni bil. 190/-
Magazeti ya Tanzania leo Oktoba 19, 2017