Hali ya utoaji wa huduma ya usomaji vitabu katika maktaba ya mkoa wa Lindi imeonekana kukumbwa na changamoto kutokana na uchakavu wa jengo la kutolea huduma hiyo.

Akizungumza na Dar24 Media Kaimu Mkutubi Mkoa wa Lindi, Mwajuma Yasini amesema kuwa uchakavu huo unahusisha paa la jengo hilo kuharibika hali inayopelekea kupitisha maji nyakati za masika hali inayohatarisha usalama wa vitendea kazi vikiwemo (vitabu na mashelf).

Amesema kuwa suala hilo linafahamika katika mamlaka husika kwa Mkurugenzi Manispaa ya Lindi na wenye mamlaka na jengo hilo ni halmashauri ingawa utekelezaji wake umekuwa hafifu.

”Suala la ukarabati wa jengo bado lipo kwenye mchakato na barua tumepeleka kwa Mkurugenzi Manispaa hadi kufikia mwezi wa sita itakuwa baadhi ya changamoto zitakuwa zimetatuliwa’’ amesema Mwajuma.

Aidha, changamoto nyingine kubwa ni watu kukosa hamasa ya kwenda kusoma katika Maktaba hiyo kutokana na wengi wao kutotambua umuhimu wa kujisomea vitabu huku wakijikita na shughuli nyingine za kijamii hali ambayo inapelekea watoto wao kujengeka katika maisha hayo.

Pia amezungumzia mikakati waliyojiwekea ili kukuza hamasa ya usomaji vitabu kwa jamii na katika taasisi mbalimbali zikiwemo shule za msingi, sekondari na vyuo, ikiwemo kuingia mikataba na walimu wao ili waweze kuwakodishia vitabu pamoja na kuboresha mabango yanayoelekeza mahali inapopatikana huduma.

Hata hivyo, Mkutubi huyo ametoa wito kwa jamii kupenda kusoma vitabu ili kuweza kujiongezea maarifa na huku akiwasihi wazazi na walezi wawe kipaumbele kwa kuwahimiza watoto wao kwenda Maktaba kujisomea.

Serikali kudhibiti taasisi binafsi na mashirika ya dini
Video: Chadema wapaza sauti kuhusu Sugu, 'Mwacheni awatumikie wananchi wake'