Mashabiki na wachezaji wa Soka duniani wanaomboleza na kutoa heshima zao kwa aliyekuwa mchezaji mpya wa Cardiff City, Emiliano Sala baada ya mwili wake kupatikana ndani ya masalia ya ndege iliyopotea mwezi uliopita.

Januari 21, Sala alikuwa akisafiri kwa ndege binafsi akitokea katika klabu yake ya zamani Nantes ya Magharibi mwa Ufaransa akielekea Cardiff kuanza rasmi kazi ya kukitumikia kikosi hicho katika Ligi Kuu ya Uingereza.

Mabaki ya ndege pamoja na mwili wa Sala yalipatikana kufuatia utafutaji wa kina uliohusisha watalaam uliofadhiliwa na watu binafsi baada ya Mamlaka za Serikali kueleza kuhitimisha zoezi la awali la utafutaji.

“Mwili umewasilishwa leo katika Bandari ya Portland na umethibitishwa na Mamlaka ya Dorset kuwa ni wa mchezaji huyo wa kulipwa, Emiliano Sala ambaye ni raia wa Argentina,” imeeleza taarifa ya Polisi.

“Familia ya Sala na rubani David Ibbotson zimejulishwa kuhusu hatua iliyofikiwa na wamekuwa wakihudumiwa kwa ukaribu na kitengo maalum cha maafa na masuala ya kifamilia, mawazo yetu yako nao katika kipindi hiki kigumu,” iliongeza taarifa hiyo.

Klabu ya Cardiff wameandika kwenye tovuti yao ujumbe wa salam za rambirambi kwa Sala na rubani David Ibbotson wakiungana na mamilioni ya salam za rambirambi kwa familia ya wawili hao zilizoandikwe kwenye mitandao, tovuti na machapisho mbalimbali.

“Kwa masikitiko makubwa, tunatoa salam zetu za rambirambi na pole kwa familia ya Sala na David. Wawili hao watabaki kwenye mawazo yetu daima,” salamu hizo zinasomeka kwa tafsiri isiyo rasmi.

Watumishi 50 wilaya ya Makete kusimamishwa kazi
Madiwani wahoji kuhusu Kondomu, 'Haiwezekani zikosekane'