Lydia Mollel – Morogoro.

Kuelekea siku ya Wanawake duniani itakayofanyika Machi 8 2024, Maofisa na Askari wa kitengo cha Dawati kutoka Jeshi la Polisi nchini, wameendelea kufanya mikutano na Wanawake kutoa elimu, huku wakiwasisiza kujiamini katika kupambania ndoto zao.

Kwa upande wake Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Malinyi, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Michael Rasha, amewataka Wanawake kutokaa majumbani na kuacha kubweteka wakisubiri kuletewa kila kitu na waume zao badala yake watoke na kuzipambania ndoto zao kwa namna yoyote ile bila kuvunja Sheria hili wawe msaada katika familia na kuongeza thamani na umuhimu wao.

Rasha ameyasema hayo wakati alipokuwa kwenye uzinduzi wa Jukwaa la Wanawake Kata ya Igawa lililofanyika katika shule ya msingi Lugala iliyopo wilaya ya malinyi.

Amesema, “ni muhimu kwa wanawake waliopo kwenye ndoa na hata wale ambao bado hawajaingia kupambania ndoto zao ili wasinyanyasike na wenza wao,kwani itawajengea uwezo wa kujiingizia kipato na kufanya maendeleo na kuacha kuwa tegemezi kwa kila kitu” Amesema Rasha.

Mkaguzi Rasha, amesisitiza kutokana na mfumo dume wa Kaya nyingi za vijijini ambapo mwanamke anaonekana kama anapaswa kutunza familia na si kufanya kazi au shughuli za kuingiza kipato ipo haja ya  wao kutambua nafasi zao na kuunganisha nguvu zao kwani Sheria na taratibu za nchi zimeelekeza kila mmoja anao wajibu Wa kufanya kazi.

Sajenti wa Polisi Mwanaisha Kubegeya, ambaye aliambatana na A/Insp Rasha ametumia jukwaa hilo kutoa elimu juu ya malezi bora kwa watoto, madhara ya mimba za utotoni, madhara ya ukatili kwa watoto pamoja na kutojichukulia sheria mkononi.

Uhalifu: Pikipiki zisizo na namba zikamatwe - Madereva Bodaboda
Maandamano ya siri yamuibua Diwani Bahi