Kundi la kigaidi linalojiita Islamic State (IS) limevamia na kushambulia bunge la Iran pamoja na jengo la kaburi la kiongozi wa kidini wa nchi hiyo, Ayatollah Khomeini linalojulikana kama Mausoleum katika mji mkuu wa Tehran ambapo watu 12 wameuawa na wengine kujeruhiwa.

Mashambulizi hayo yamefanyika leo kwa wakati mmoja. Vyombo vya dola vya ilani vimeeleza kuwa washambuliaji watano wenye silaha waliingia ndani ya jengo la bunge, na mmoja alijitoa mhanga kwa kujilipua kwa bomu. Aidha, ripoti zimeeleza kuwa magaidi waliingia ndani ya bunge hilo kupitia mlango wa raia wakiwa wamevalia mavazi ya kike.

Mtoto akishushwa kupitia dirishani, kwenye jengo la bunge la Iran

Hata hivyo, wanausalama walifanikiwa kuzima mashambulizi hayo baada ya saa kadhaa za kusikika milio ya risasi. Kituo cha runinga cha Iran kimeripoti kuwa washambuliaji wote waliuawa na wanausalama.

Magaidi wa IS wametoa tamko kukiri kutekeleza shambulizi hilo likiwa ni shambulizi la kwanza ndani ya Iran na kutishia kuwa wataendelea kutekeleza mashambulizi mengine wakilenga  waumini wa Shia ambao ni wengi.

Rais wa Iran, Hassan Rouhani amesema kuwa ugaidi ni tatizo la dunia nzima na kutoa wito kwa mataifa yote kushirikiana kuendesha vita dhidi ya ugaidi.

Iran imekanusha kuwepo kwa utekaji au kushikiliwa kwa watu ndani ya jengo la bunge wakati wa mashambulizi hayo.

Magazeti ya Tanzania leo Juni 8, 2017
Taifa Stars yawasili nchini ikitokea Misri, Msuva aahidi watanzania