Benki ya dunia (WB) na shirika la fedha duniani (IMF) wametoa wito kwa mataifa 20 tajiri zaidi duniani (G20), kusamehe madeni ya nchi maskini.

Rais wa Benki ya Dunia David Malpass ameeleza hayo kwenye mkutano na waandishi wa habari uliofanyika Oktoba 12, ambapo amesema kuwa mataifa ya G20 ni vyema waongeze mwaka kwa mataifa maskini ili kupunguza madeni.

Malpass amesema baadhi ya wakopeshaji kutoka nchi zilizoendelea, bado wanasita kurefusha kwa mwaka mmoja, kipindi cha kusamehe madeni kwa nchi maskini zilizoathiriwa na janga la Virusi vya Corona.

Malpass amesema wakopeshaji wa G20 hawajafikia makubaliano kuhusu pendekezo la benki ya dunia na IMF, la kurefusha kipindi cha mwaka mmoja kwa mataifa maskini ili yaweze kulipa madeni yao.

Aidha kiongozi huyo wa benki ya Dunia amesema huenda wiki hii wakopeshaji hao wakaafikiana kuzisamehe nchi maskini kulipa madeni kwa kipindi cha miezi sita.

Ameongeza kuwa ataendelea kuomba misaada zaidi ya pesa itolewe kwa nchi za Afrika, baada ya nchi nyingi kuathiriwa na virusi vya corona.

Mawaziri wa fedha na wakuu wa benki za Taifa kutoka kundi la G20, wanatarajiwa kufanya mkutano kwa njia ya video kesho Oktoba 14, ili kuchukua maamuzi.

Ronaldo akutwa na Corona
TFF yashindwa kutoa uamuzi sakata la Morrison