Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa amemteuwa Gwiji wa Soka la Bongo Ally Mayay Tembele kuwa Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo.

Ally Mayay ambaye aliwahi kucheza soka katika klabu za CDA ya Dodoma na Young Africans ameteuliwa kushika wadhifa huo, akichukua nafasi ya Yusuph Omary Singo aliyepangiwa majukumu mengine na uteuzi huo umeanza kazi rasmi leo Septemba 20, 2022.

Barua ya uteuzi wa Ally Mayay imeeleza: Katika kuimarisha utendaji kwenye Sekta ya Maendeleo ya Michezo Nchini na kufuatia maelekezo ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Mohamed Mchengerwa, ya kufanya maboresho ili kuongeza tija, Wizara inamtambulisha, Bw. Ally Mayay Tembele kuwa Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo nchini wakati taratibu nyingine zikiendelea.

Bw. Mayay ambaye ni Afisa Mwandamizi katika Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini, amehamishiwa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na kuruhusiwa kukaimu majukumu haya kwa mujibu wa kibali cha Ofisi ya Rais Utumishi kupitia barua yenye kumbukumbu namba CCD.273/311/01/W/45 cha tarehe 15 Septemba 2022.

Uteuzi huo wa Bw. Mayay ambaye anachukua nafasi ya Bw. Yusuph Omary Singo aliyepangiwa majukumu mengine unaanza leo Septemba 20, 2022.

Wadau wa Michezo wanaombwa kumpa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yake.

Bungeni: Serikali yatangaza kufuta tozo
Serikali yathibitisha uwepo wa Ebola, mmoja afariki