Wananchi wametakiwa kuwa makini na mtu au taasisi binafsi zinazopita na kuwadanganya kwa kuwatoza fedha za usajili wa kikundi kwa ajili ya kufaidika na mpango wa Millioni 50 kwa kila kijiji kama zilivyoahidiwa na Serikali ya awamu ya tano.

Akizungumza na  waandishi wa habari Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi  Bi. Beng’i Issa amesema kuwa kuna taasisi binafsi zimejitokeza na kuwatoza fedha za usajili wa kikundi ili kuweza kufaidika na mradi huo kinyume na taratibu za Serikali.

Bi. Issa amesema kuwa hivi karibuni kumekuwa na taarifa kutoka sehemu mbalimbali nchini kuwa baadhi ya taasisi na watu binafsi wanawadanganya wananchi kuwa mpango wa shilingi milioni 50 kwa kila kijiji zitapitia kwenye taasisi zao na kuwatoza wananchi fedha za usajili.

“Wananchi wasirubuniwe na kutoa fedha za usajili kwa ajili ya kupata fedha za mradi huo kwani hakuna malipo yoyote na bado ugawaji huo haujaanza” alisema Bi. Issa.

Aidha Bi. Issa amesema kuwa mradi huo bado haujaanza kutolewa kwa kuwa  Serikali bado inapanga utaratibu wa kuwafikia wananchi wa vijiji vyote nchini ili  kunufaika na mradi huo.

Mbali na hayo Bi. Issa ametoa rai kwa watanzania wasihadaike na taasisi hizo na kutoa onyo kali kwa yeyote atakayebainika kujihusisha na zoezi hilo hatua kali zitachukuliwa zidi  yake.

Mamlaka Ya Bandari Yakanusha Kuwa Na Mvutano Na Wamiliki Wa Bandari Kavu Nchini
Serikali Yajiandaa Kutangaza Zabuni Ya Kujenga Kijiji Cha Michezo Temeke