Timu ya taifa kwa Wanawake wenye umri chini ya miaka 17 ‘Serengeti Girls’ mwezi Septemba itasafiri kwenda nchini Uingereza kuweka kambi maalumu kwenye viwanja wa Southmpton kujifua kwaajili ya Kombe la Dunia litakalofanyika Oktoba, 2022 nchini India.

Hayo yamesemwa leo Jumatatu (Agosti 29) na Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Hassan Abbas akifungua semina ya Bodi ya Ligi kwa Wanahabari jijini Dar es Salaam.

Abbas ameeleza Serikali imeweka mipango mkakati ya kuzihudumia timu za taifa kwa kila mchezo ikiwemo Serengeti Girls ambayo mwezi ujao itasafiri hadi Uingereza.

“Ukiangalia kwa sasa serikalini kila eneo kunagusa michezo, timu zote za taifa tunazisapoti kadri tuwezavyo na tutaendelea kufanya hivyo kwa ubora zaidi,” amesema Abbas na kuongeza;

“Mfano mwezi ujao Serengeti Girls inaenda kuweka kambi England katika viwanja vya timu ya Ligi Kuu nchini humo Southamptom.

Sio jambo dogo, ikiwa huko itacheza mechi mbalimbali za kirafiki na timu kubwa kubwa za Wanawake kisha itaenda Uarabuni kuendelea na kambi kabla ya kwenda India kwenye mashindabo.”

Abbas pia ameeleza Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo imeendelea kutafuta vyanzo vya mapato kuhakikisha inakuwa imara zaidi kiuchumi.

“Kwa sasa tunapata asilimia tano kutoka katika michezo ya kubahatisha na tunaendelea kutafuta vyanzo vingine vingi lengo ikiwa ni kuwa imara zaidi kiuchumi na kusapoti michezo kwa ujumla.”
Mwaka huu itakuwa mara ya kwanza kwa Serengeti Girls kushiriki Kombe la Dunia.

Waziri Mkuu aombwa kujiuzulu kwa 'kukata mauno' hadharani
UNHCR yasifu ukarimu na ulinzi wa Tanzania