Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo Januari 16, 2022 amekagua maendeleo ya ujenzi wa Ikulu inayojengwa katika eneo la Chamwino, Jijini Dodoma na kusema ameridhishwa na kasi ya ujenzi na ubora wa majengo hayo akimtaka mkandarasi ahakikishe mradi huo unakamilika mwezi mei mwaka huu.

Waziri Mkuu akizungumza na viongozi wasimamizi wa ujenzi wa Ikulu ya Chamwino

Waziri Mkuu amewasisitiza wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha mradi huo kwa wakati na kuwapongeza wote wanaohusika na ujenzi. “Tunataka kumuwezesha Mheshimiwa Rais kufanya kazi katika eneo lake maalum na afanye kazi katika mazingira mazuri na kwa ufanisi.”

“Nimefurahishwa na taarifa kwamba ujenzi huu umefikia asilimia 91 na hatua iliyobaki hizi asilimia 9 ni kazi ndogondogo kama uwekaji wa milango, njia za mifumo ya hewa na umeme na zote zinaenda vizuri.” Waziri Mkuu amesema kuwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan pia anatarajia kuona ujenzi huo unakamilika kwa wakati.

Waziri Mkuu amelipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kutekeleza ujenzi huo kwa ufanisi. “Ramani iliyoko hapa iko sawasawa na jengo la Ikulu lililoko Dar es Salaam, Wakandarasi wetu mmefanya kazi kubwa sana, Hii imedhihirisha kuwa nchi yetu ina wataalam wa kutosha kujenga aina yoyote ya majengo.”

Waziri Mkuu akizungumza na vikosi vya JWTZ vinavyosimamia ujenzi wa Ikulu ya Chamwino.

Kwa Upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania, Mhandisi Daudi Kondoro amemhakikishia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba mradi huo utakamilika na kukabidhiwa mwezi Mei kama inavyotarajiwa kwani sasa uko katika hatua za mwisho za ukamilishaji.

Milionea mtoto anaetarajiwa kustaafu na miaka 15
Habari kubwa kwenye magazeti leo, Januari 17, 2022