Kaka wa aliyekuwa mbunge wa jimbo la Singida Mashariki kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, Alute Mughwai amesema kuwa kesi ya maombi iliyofunguliwa na Lissu sio ya hovyo kama inavyozungumziwa na upande wa serikali.

Ameyasema hayo jijini Dar es salaam mara baada ya majibizano makali ya kisheria kutokea mahakamani, ambapo upande wa serikali ulipeleka mawakili 15 kwa ajili ya kuweka pingamizi dhidi ya kesi ya Tundu Lissu.

Amesema kuwa kesi hiyo ina umuhimu mkubwa ndiyo maana upande wa serikali umepeleka mawakili 15 ikiwa ni pamoja na mwanasheria mkuu, hivyo kuonyesha kuwa kesi hiyo ina umuhimu wa kipekee kwa mustakabali wa nchi.

”Tunataka mahakama itueleze kama ni sahihi kwa mbunge wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushambuliwa mchana kweupe, halafu hapewi huduma ya matibabu, baada ya hapo anaondolewa ubunge, kwa hoja kwamba hayupo bungeni na hawajui alipo,”amesema Mughwai

Hata hivyo, maombi hayo ya Lissu ambayo yalitakiwa kuanza kusikilizwa hapo jana mbele ya Jaji Sirilius Matupa, hayakusikilizwa baada ya upande wa serikali kuwasilisha pingamizi la awali lenye hoja tisa kutaka shtaka hilo lifutiliwe mbali.

Waziri Mkuu aagiza DED achunguzwe
Ndege ya Air Tanzania yazuiliwa Afrika Kusini