Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuondoka nchini leo jioni (Jumanne, Mei 10, 2016) kwenda London, Uingereza kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi unaojadili suala la kupambana na rushwa (Anti-Corruption Summit 2016) utakaofanyika Mei  12, mwaka huu.

 

Akizungumza na waandishi wa habari leo mchana, Waziri Mkuu alisema anaenda kumwakilisha Mheshimiwa Rais, Dk. John Pombe Magufuli kwa sababu siku hiyo hiyo, atalazimika kuhudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais wa Uganda, Mhe. Yoweri Museveni.

 

“Mheshimiwa Dk. Magufuli ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), na siku hiyo hiyo, mmoja wa marais wa nchi wanachama anaapishwa. Kwa hiyo amelazimika kwenda kuhudhuria sherehe hizo,” alifafanua Waziri Mkuu.

 

Akizungumzia kuhusu mada ya mkutano huo, Waziri Mkuu amesema Tanzania inafanya vema katika mapambano dhidi ya rushwa na kwamba baadhi ya nchi zimeanza kuvutiwa na juhudi ambazo Serikali imekuwa ikichukua.

 

“Waziri Mkuu wa Uingereza ameandaa mkutano huu na alimwalika Mheshimiwa Rais Magufuli ili ahudhurie akiwa ni miongoni wa wakuu wa nchi 60 watakaohudhuria mkutano huo. Tanzania ni miongini mwa nchi mbili kutoka bara la Afrika ambazo zimealikwa kushiriki. Nchi nyingine ya kutoka Afrika ni Nigeria,” alisema.

 

Waziri Mkuu atafuatana na Jaji Mkuu wa Tanzania, Othman Chande, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kimataifa na Kikanda, Balozi Dk. Augustine Mahiga, Mkurugenzi wa TAKUKURU, Bw. Valentino Mlowola, wataalamu wa sekta ya rushwa na wanasheria

Video Mpya: Nay wa Mitego – Saka Hela
SERIKALI KUAGIZA TANI 70,000 ZA SUKARI