Beki wa zamani wa Simba SC, Pascal Wawa anaitumia fursa ya kukaa nje ya kazi kwa sasa akisomea ukocha ngazi ya Grassroot, inayoendeshwa na Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Ilala (IDFA).

Mchezaji huyo amefichua kuwa miongoni mwa sababu zilizomshawishi kusomea ukocha ni kupata maarifa ya mchezo huo anayoamini yatamsaidia kwenye kazi zake kabla na baada ya kustaafu soka.

Wawa amesema kwamba baada ya kutangazwa kozi hiyo hakusita kuchangamkia fursa anayoamini imebeba maono ya baadaye kuwa kocha.

“Siwezi kuacha fursa kama hiyo mbele yangu, kwanza imekuja kipindi kizuri ambacho nilikosa timu. Naamini nitakapoanza kucheza kutakuwa na vitu vipya ambavyo vimeongezeka,” amesema wawa

“Natarajia nikija kustafu soka, nitakuwa kocha ndio maana nimeanza kujiwekea misingi ya ndoto zangu zijazo, pamoja na hilo mchezaji yeyote anaweza akasomea kwa faida ya kupata maarifa ya namna ya kucheza kwa utalaamu zaidi.”

Mbali na hilo amejibu swali aliloulizwa anawaonaje mabeki wa Simba SC, Henock Inonga na Che Malone? Alijibu: Ni mabeki wazuri. wanahitaji kufokasi kuipambania timu yao.”

Wawa aliyeichezea Simba 2017-2020 aliisaidia kunyakua mataji manne ya Ligi Kuu Bara(2017/18, 2018/19, 2019/20 na 2020/21) kisha akatimkia Singida Fountain Gate ambako hakucheza kwa muda mrefu.

Habari kuu kwenye Magazeti ya leo Machi 15, 2024
Tabora United kugoma Ligi Kuu