Kiungo wa timu ya Yanga Haruna Niyonzima ameanza mazoezi na wachezaji wenzake kujiandaa na mechi ya Kombe la FA.

Keshokutwa Yanga itashuka dimbani kuikabili Friends Rangers ya Magomeni katika mechi ya FA.

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo kwenye uwanja wa Karume jijini Dar es salaam,Kocha msaidizi wa Yanga Juma Mwambusi alisema wamempokea Haruna na wataendelea kumtazama katika mazoezi ya kesho na huenda wakamtumia kwenye mchezo wa Jumapili endapo wataridhishwa na kiwango chake.

“Kama hatutoridhishwa na kiwango hatutomtumia Jumapili na badala yake tutampa mazoezi zaidi,”alisema Mwambusi.

Kwa upande wake Haruna ameahidi kufanya vizuri zaidi mara baada ya kurejea tena kundini.

Hivi karibuni Yanga ilitangaza kuvunja mkataba wa kiungo huyo kwa madai kwamba alikiuka masharti ya mkataba huo kwa kuchelewa kujiunga na kambi.

Hata hivyo Yanga ilibadilika na kumshinikiza Niyonzima aombe radhi kwa mashabiki na wanachama wa timu hiyo huku uongozi ukisisitiza kwamba mchakato wa kuhakikisha mchezaji huyo anarudi kundini unaendelea vizuri.

Sakata la kiungo huyo bado linazua maswali mengi kwa wapenzi wa timu hiyo kwamba ni kweli mkataba umevunjwa? Kama ni kweli kwanini aendelee kucheza sasa badala ya kusubiri dirisha lijalo la usajili ili taratibu za mkataba zianze upya?

Picha: Kishindo cha Amiri Jeshi Mkuu kuwatumbua Wakuu wa Mikoa
Ashanti Utd Yaondolewa Kombe La Shirikisho