Kocha Mkuu wa USM Alger Benchikha Abdelhak amesema bado ni 50 kwa 50 kwa kikosi chake kutwaa ubingwa wa Kombe la Shirikisho Barani Afrika, licha ya kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Young Africans jana Jumapili (Mei 28).

Young Africans ilikuwa nyumbani Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam ikishuhudiwa na Mashabiki na Wanachama wake, lakini ilishindwa kufurukuta, na sasa inajipanga kwenya kujiuliza kwenye mchezo wa Mkondo wa Pili utakaopigwa Jumamosi (Juni 03) nchini Algeria.

Kocha Benchikha amesema inafurahisha kushinda ugenini, lakini bado wana kazi kubwa katika mchezo wa Mkondo wa Pili ambao anaamini utakua mgumu zaidi, kwa sababu utakwenda kuamua nani atakuwa Bingwa wa Kombe la Shirikisho msimu huu.

Amesema hata Wapinzani wao Young Africans bado wana nafasi ya kufanya vizuri katika Uwanja wa ugenini kwani wamewahi kufanya hivyo mara kadhaa msimu huu katika Michuano hiyo, hivyo hana budi kukiandaa vyema kikosi chake kwa ajili ya kupambana nyumbani kwa kulinda ushindi wa 2-1 na ikiwezekana kusaka ushindi mwingine.

 “Tunarudi Algeria lakini bado mechi haijaisha, ni asilimia 50 kwa 50. Bado tuna kazi ya kufanya Algeria kwa sababu katika mechi ya marudiano Young Africans hawana cha kupoteza. Watacheza wanavyojua ili wapate matokeo. ”

“Ninaamini utakua mchezo mgumu kwa kila upande lakini kwetu tutapaswa kucheza kwa uangalifu mkubwa kwa sababu tutalazimika kulinda ushindi wetu, huku tukisaka ushindi mwingine katika Uwanja wetu wa nyumbani.”

“Nina uhakika tutajiandaa vizuri kwa ajili ya kupambana katika mchezo huo ambao tutakuwa nyumbani In Shaa Allah.” amesema Benchikha

Katika mchezo wa Mkondo wa Pili, Young Africans italazimika kusaka ushindi wa mabao 2-0 ama zaidi ili kujihakikishia Ubingwa wa Kombe la Shirikisho Barani Afrika, huku wenyeji wao USM Alger wakihitaji sare ama ushindi wa aina yoyote kutawazwa kuwa Mabingwa.

Tinubu kuapishwa rasmi leo, Rais Samia awasili kushuhudia
Mataifa yaonya mlipuko fangasi ya uti wa mgongo