Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Juni 18, 2021 imemfutia mashtaka na kumwachia huru mfanyabiashara  Marijan Msofe (53) maarufu Papaa Msofe na wenzake wanne.

Hayo yamejiri baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kuwasilisha hati mahakamani hapo akieleza kuwa hana nia ya kuendelea na shauri hilo dhidi ya washtakiwa hao.

Msofe na wenzake walikuwa wanakabiliwa wa mashtaka matano likiwemo la kujipatia Sh943 milioni kwa njia ya udanganyifu, katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 124/2019 ni Wenceslaus Mtu(49), Mwesigwa Mhingo (36), Josephine Haule (38) na Fadhil Mganga (61).

Uamuzi wa kuwafutia kesi hiyo na kuwaachia huru washtakiwa hao imetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Huruma Shaidi wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya kutajwa.

Awali, wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai kuwa DPP ameieleza mahakama hiyo kuwa hana nia ya kuendelea na shauri hilo.

Baada ya upande mashtaka kueleza hiyo, Shaidi alikubaliana na ombi hilo na kuwafutia mashtaka na kuwaachia huru.

Katika kesi hiyo, washtakiwa wanadaiwa kuratibu, kuongoza genge la uhalifu, utakatishaji fedha na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.

Miongoni mwa mashtaka yao ni kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu ambapo washtakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Desemba 2018 na Septemba 2019 jijini Dar es Salaam.

Inadaiwa kuwa wakiwa na nia hiyo walijipatia dola za Marekani 300,000 (Sh 660milioni) kutoka kwa Pasca Camille wakidaiwa kuwa watamuuzia dhahabu yenye uzito wa kilo 200 ambayo wangemsafirishia kwenda Ureno wakati wakijua si kweli.

Kwa mara ya kwanza washtakiwa hao walifikishwa Kisutu Desemba 2, 2019 wakikabiliwa na mashtaka hayo.

Zambia yatangaza maombolezo ya siku 21
Video: Harmonize afunguka ya Kajala