GWIJI wa soka duniani Edson Arantes do Nascimento ‘Pele’ ametuma salamu za rambirambi kufuatia msiba wa nahodha na kiungo mshambuliaji zamani wa timu ya taifa ya Argentina, Diego Armando Maradona.

Maradona alifariki dunia juzi Jumatano (Novemba 25) akiwa na umri wa miaka 60, huku taarifa za kifo chake zimethibitishwa na Shirikisho la soka nchini Argentina kupitia kwa Rais wake Claudio Tapia.

Pele ametuma salamu za rambirambi akisema, “Pengine siku moja tutacheza pamoja mpira juu mawinguni,” amesema Pele katika taarifa yake fupi iliyotolewa na wawakilishi wake na ikinukuliwa na Shirika la Habari la Reuters.

Maradona hivi karibuni alikuwa akikabiliwa na matatizo mengi ya kiafya huku akilazwa mara kadhaa.

Na Jumatano, Novemba 25 akiwa nyumbani kwake jijini Buenos Aires, mshindi huyo wa Kombe la Dunia mwaka 1986 akiwa na Argentina alifariki dunia kwa mshtuko wa moyo.

Rais wa Argentina, Alberto Fernandez ametangaza siku tatu za maombelezo ya kitaifa kutokana na kifo cha Maradona.

Mapema mwezi huu, nyota huyo alifanyiwa upasuaji wa ubongo kwa ajili ya kutoa damu ilikua imeganda, na baadaye akaruhusiwa kutoka hospitali juma lililopita.

Baada ya upasuaji huo, ilitangazwa kuwa Maradona angeanza matibabu ya uraibu wa pombe.

Azam FC yataja sababu ya kusitisha mkataba
Habari kubwa kwenye magazeti leo, Novemba 27, 2020