Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amepiga marufuku Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na wakandarasi wake kununua nguzo za umeme kutoka nchi za nje wakati nguzo hizo zinazalishwa kwa wingi na wawekezaji wa ndani.

Profesa Muhongo alitangaza marufuku hiyo alipofanya ziara mkoani Njombe hivi karibuni na kutembelea kiwanda cha kuzalisha umeme unaotokana na mazao ya miti.

“Tuna miradi mingi, wakandarasi wameenda kununua nguzo Uganda, wamenunua nguzo Kenya, wamenunua nguzo Zimbabwe na sasa hivi wananunua nguzo nyingi kutoka Afrika Kusini. Sasa tumemsikia ndugu yetu pale ana nguzo… kwa hiyo lazima hicho kikao chenu na nyie Mkoa mwende pale,” alisema Profesa Muhongo.

“Mkinunua hizo nguzo kwanza nyie mtapanua mashamba, wakulima watapata kazi. Na kuna wengine wakulima wa miti waliopanda miti wanavuna wanaweza wakakiuzia hicho kiwanda (cha kufua umeme),” alisema.

Waziri huyo wa nishati pia alikitaka kiwanda hicho pia kupunguza bei ya umeme kinacholiuzia shirika hilo.

 

Thomas Ulimwengu Aeleza Anavyojiandaa Kwenda Ulaya
Washindi wa Tuzo za Golden Globes 2016 wako hapa