Waziri Mkuu, Kassim Mjaliwa amewasili wilaya ya Hanang Mkoani Manyara na kukutana na viongozi wa mkoa huo na kupokea taarifa ya hali halisi ya tukio la maafa, lilotokea jana Desemba 3, 2023 na kusababisha vifo na majeruhi.

Majaliwa ametoa pole kwa Viongozi na wananchi wa Hanang kwenye kikao kilichofanyika leo jumatatu Novemba 4, 2023 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mawaziri, Naibu Waziri, Makatibu wakuu vyombo vya ulinzi na Usalama na watendaji wa Taasisi za Serikali.

Amesema tukio la jana linafanana na tukio jingine lililowahi kutokea mwaka 1990 katika eneo la Ndanda ambako mlima uliporomoka na kusomba nyumba na barabara, hali ambayo ilisababisha vifo na majeruhi.

Aidha, Majaliwa pia amezishukuru kamati za maafa za wilaya ya Mkoa ambazo zilianza kuchukua hatua za uokoaji tangu jana lakini pia Mawaziri na watendaji wao ambao walikuja kutoa msaada kwa kuungaa na viongozi wa Mkoa wa Manyara.

Amesema, matibabu yanaendelea kutolewa kwa majeruhi ambapo timu ya madaktari bingwa kutoka Dodoma, Singida na Arusha imeungana na kuanza kutoa huduma za upasuaji kwa wagonjwa watatu waliovunjika mifupa.

Hata hivyo, Waziri Mkuu pia ameeleza kuwa tayari majeneza yameagizwa kutoka babati na singida ili ndugu waliotambuliwa waweze kuhifadhiwa kwenye nyumba zao za milele, hata hivyo Waziri Mkuu anatarajiwa kushiriki kuaga miili ya marehemu.

Kinana awapa uhakika Wananchi janga la mafuriko
Sesanga atangaza kumuunga mkono Katumbi