Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Julius Mtatiro amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, kumhamishia shule ya mjini Mwalimu Judith Sichalwe (29,) ambaye amejifungua mapacha wanne.

Mtatiro ametoa maagizo hayo baada ya kumtembelea Mwalimu huyo katika kijiji cha Mkapunda kilicho umbali wa kilomita 100 kutoka Tunduru Mjini, na kusema Serikali itakuwa jirani na Mwalimu huyo ili kujua maendeleo ya afya yake na watoto.

Amesema ni wajibu wa Serikali kumpa usaidizi utakaompa nafuu mwalimu huyo, kwani upo uwezekano wa kushindwa kumudu gharama za maisha kutokana na kupata idadi ya watoto wachanga wanne kwa wakati mmoja na kuwataka Watanzania watakaouguswa na tukio hilo kutoa msaada ili aweze kuwatunza.

“Watanzania watakaoguswa kumsaidia Mwalimu Judith wasisite kuwasiliana naye kupitia namba 0673 103 536 iliyosajiliwa kwa majina Judith Sichwale, kwani anahitaji msaada kutokana na idadi ya watoto aliowapata na maziwa ya mama pekee hayataweza kutosha kuwahudumia wote,” amesema Mtatiro.

Awali, akiongea baada ya kutembelewa na ugeni Mwl. Judith amesema, amepata mapacha wanne wawili wakiwa ni jinsia ya kiume na wawili wakike na kwamba alijifungua kwa njia ya kawaida katika Hospitali ya Misheni ya Mbesa iliyopo Mkoani Mkoani Ruvuma.

“Namshukuru sana Mungu kwa kuniwezesha kujifungua salama,vlakini kutokana na mahitaji makubwa ya watoto, nawaomba wasamaria wema wanisaidie mahitaji mbalimbali kama fedha na maziwa ili niweze kuwalea hawa watoto,”amefafanua Mwalimu Chawe.

Tayari upande wa watumishi wenzake wameanza kujitolea kwa kujichangisha kiasi cha fedha, ili Mwalimu huyo aweze kumudu jinsi ya kuwalea watoto hao ambao wanahitaji uangalizi wa karibu na chakula katika ukuaji wao.

Geita Gold: Tutamlipa kwa wakati Ndayiragije
Ahmed Ally aisasambua Young Africans