Nahodha wa klabu ya Simba, John Bocco amesema wachezaji wote wa Simba wanatambua kuwa wamebaki na njia moja tu ya kushiriki michuano ya kimataifa mwakani ambayo ni kuchukua ubingwa msimu huu.

Ameyasema hayo mapema hii leo kwenye hafla fupi ya chakula cha mchana iliyoandaliwa na mashabiki wa klabu hiyo ikiwa ni maalum kwa kuwapokea wachezaji waliotua leo nchini wakitokea Misri ambapo walicheza mchezo wa Kombe la shirikisho.

“Tunatambua tumetoka kwenye mashindano yote, kwaniaba ya wachezaji wenzangu tunawashukuru mashabiki na tunaahidi kuwa nafasi pekee tuliyonayo ili tushiriki kimataifa tunatakiwa kuchukua ubingwa wa ligi na kulinda ukubwa na heshima ya Simba”, amesema Bocco.

Aidha, Simba imetolewa na Al Masry kwa mabao ya ugenini baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaam kabla ya jumamosi kutoa suluhu nchini Misri hivyo kuondolewa kwenye michuano ya kombe la shirikisho.

Hata hivyo, Klabu hiyo kwasasa inaongoza msimamo wa ligi ikiwa na alama 46 sawa na Yanga zikitofautiana idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa pamoja na idadi ya michezo Yanga ikiwa mbele kwa mchezo mmoja.

 

Kikwete: Viongozi Simba SC, Young Africans mjitathmini
JPM awashangaa wanaohoji viwanda