Aliyekuwa mgombea Mwenza wa Rais kwa tiketi ya Chadema, Juma Haji Duni ambaye wiki hii amerejea katika chama chake cha awali cha CUF amekosoa muundo wa uongozi wa chama hicho alichojiunga nacho mwaka jana ili kutimiza matakwa ya sheria na taratibu za uchaguzi mkuu.

Akiongea katika mahojiano maalum na kituo cha runinga cha Azam Two, Duni ameeleza kuwa muundo wa uongozi wa Chadema una urasimu mkubwa unaosababisha kila kiongozi katika ngazi fulani kujiona mkubwa na anayeweza kutoa maamuzi yake.

“Ule muundo wake wa kiutawala ni mkubwa mno, bureaucracy ni ndefu sana kiasi kwamba kila mmoja kule ni kambare ana sharubu. Kule kuna [ngazi] Taifa, kuna Kanda, kuna Mkoa, kuna Wilaya, kuna Jimbo. Sasa uamuzi unaweza ukatoka Taifa lakini mtu wa Jimbo akasema huo uamuzi mimi siukubali,” alisema Haji Duni.

Alisifafanua kuwa muundo huo mrefu wa uongozi unachelewesha na kukwamisha maamuzi yatokayo katika ngazi ya Juu.

Katika hatua nyingine, Mwanasiasa huyo alisisitiza kuwa kuna faida kubwa waliyoipata kutokana na kuunda Ukawa na kwamba ndio njia pekee ya kuiondoa CCM madarakani.

“Kitu kimoja ambacho nakiamini ni kwamba bila Ukawa hatuwezi kuiondoa CCM. Na matokeo ya mwaka huu yameonesha kwamba Chama cha CUF hakijawahi hata mara moja kwa miaka 20 iliyopita kupata viti vingi bara, kupata madiwani wengi Bara na kupata Halmashauri hadi Halmashauri ya Tanga ambayo tumenyang’anywa kwa nguvu,” alisema.

Alifafanua kuwa hali hiyo inaonesha dhahiri kuwa wapinzani wakishirikiana wanaweza kuiondoa CCM madarakani.

Dk. Slaa: Tutaheshimiana tu
Baada ya kumtimua Anne Kilango, Magufuli awasaka Mawaziri, awarekodi kwa siri